1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chama cha AfD champiga marufuku mgombea wake mkuu wa EU

23 Mei 2024

Chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha AfD cha nchini Ujerumani, kimempiga marufuku mgombea wake mkuu katika uchaguzi wa bunge la Ulaya

https://p.dw.com/p/4gAVD
Karikatur | Le Pen & AfD
Picha: DW

Chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha AfD cha nchini Ujerumani, kimempiga marufuku kujitokeza hadharani mgombea wake mkuu katika uchaguzi ujao wa bunge la Ulaya, Maximilian Krah, kufuatia matamshi yake kwamba siyo wanachama wote wa kundi la kijeshi la SS lililohudumu chini ya Adolf Hitler na chama cha Wanazi walikuwa wahalifu.

Msemaji wa chama cha AfD amethibitisha ripoti iliyochapishwa katika Gazeti la Bild jana Jumatano, kwamba kamati kuu ya shirikisho imempiga marufuku Krah kuhutubia mikutano ya hadhara kuelekea uchaguzi wa bunge la Ulaya mwezi ujao.

Soma pia: Mahakama: AfD na tawi lake la vijana ni washukiwa wa misimamo ya Itikadi kali.

Krah alisema kupitia mtandao wa kijamii wa X kwamba atajizuwia kushiriki kampeni zaidi na atajiuzulu kuwa mwanama wa kamati kuu ya shirikisho ya chama hicho.

Hatua hiyo imekuja baada ya chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha Ufaranda, cha National Rally, kusema hakitaki tena kukaa katika kundi moja la bunge la AfD baada ya matamshi ya Krah.