1. Inhalt
  2. Navigation
  3. Weitere Inhalte
  4. Metanavigation
  5. Suche
  6. Choose from 30 Languages

Habari za Ulimwengu

Taarifa ya Habari za Ulimwengu kutoka Idhaa ya Kiswahili ya DW

News | 08.02.2012 | 16:03

Umoja wa nchi za Kiarabu wautaja ujumbe wake kuondoka Syria

Umoja  wa  nchi  za  Kiarabu, Arab League,  umeutaka ujumbe  wake  wa  uangalizi  kuondoka  nchini  Syria. Hayo  yamethibitishwa  na  makao  makuu  ya  umoja  huo mjini  Cairo, ambapo  mataifa  kadha  ya  Kiarabu kutokana  na  kuendelea  kwa  ukandamizaji  wa  serikali ya  nchi  hiyo  dhidi  ya   wapinzani  yameomba kuondolewa  kwa  waangalizi  wake. Waangalizi  hao waliingia  nchini  humo  mwezi  Desemba  kwa  masharti ya  kuangalia  kuondoshwa  kwa  jeshi  katika  miji  na kuachiliwa  huru  kwa  wafungwa  wote  wa  kisiasa  nchini humo. Kwa  mujibu  wa  wanaharakati,  jeshi  la  Syria  kwa muda  wa  siku  ya  tano  mfululizo  limepambana  na waasi  katika  mji  wa  Homs. China  na Urusi zimepinga azimio la  baraza  la  usalama  la  umoja  wa  mataifa , lililokuwa  na  lengo  la  kuilazimisha  serikali  ya  nchi  hiyo kuacha kupambana  na  wapinzani. Shirika  linalochunguza   ukiukaji  wa  haki  za  binadamu nchini  Syria  limesema   kuwa  kutokana  na  mashambulio ya  risasi  na  makombora  katika  maeneo  yanayoishi watu,  watu  kadha   wameuwawa. Katika   mapambano dhidi  ya  mji  wa  Homs  tangu  mwishoni  mwa  juma  zaidi ya  watu  200  wameuwawa.

Ugiriki kutoa jibu kuhusu mipango ya kubana matumizi

Viongozi  wa  serikali  ya  muungano  nchini  Ugiriki wanatayarisha  jibu  lao  kuhusiana  na  mswada  wa kubana  zaidi  matumizi , ambapo  wakopeshaji  wanadai  ili kuweza  kuidhinisha  kiasi  cha  euro  bilioni  130  za uokozi  ambazo  zitaisaidia  nchi  hiyo  kuepuka uwezekano  wa  kushindwa  kulipa  madeni  yake mwezi ujao. Uamuzi  utatangazwa  katika  mkutano  na  waziri  mkuu Lucas Papademos, ambao  ulipangwa  kufanyika  mchana wa  leo  na  kuahirishwa. Hii  itatoa  kwa  vyama  vitatu vinavyounda  serikali  muda  zaidi  kupitia  waraka  wenye kurasa  50  , ambao  umetayarishwa  na wataalamu  wa kundi  linaloidai  nchi  hiyo  jana Jumanne. Bila  ya  kupata  mkopo  huo , Ugiriki  haitakuwa  na  fedha za  kutosha  kulipia faida  kwa  walionunua  dhamana mwezi  ujao, na  kuzusha  hali  ya  kushindwa  kulipa madeni  na  kufilisika   na  kuleta  hali  ya  mtikisiko  katika masoko  ya  fedha  pamoja  na  uchumi  wa  dunia.

Waungaji mkono wa rais wa zamani waandamana

Male. Waungaji  mkono  wa  rais  wa  zamani  wa  Maldive , Mohammed Nasheed, wamefanya  ghasia   mitaani  katika mji  mkuu  wa  nchi  hiyo  leo  wakiwarushia  polisi mabomu  ya  petroli.  Wanadai  rais  huyo  arejeshwe madarakani. Ghasia  hizo  zilizuka  baada  ya  mtu aliyechukua  nafasi  ya  Nasheed , rais  Mohammed Waheed Hassan , kutoa  wito  kuunda  serikali  ya  umoja wa  kitaifa   kumaliza  mzozo  wa  kisiasa   ambao umeivuruga  nchi  hiyo  kwa  miezi  kadha  sasa. Nasheed  amesema  kujiuzulu  kwake   jana  Jumanne ilikuwa  ni  mapinduzi  na  kwamba  ameondolewa madarakani  baada  ya  kulazimishwa  kwa  mtutu  wa bunduki. Ametaka  rais  mpya  Hassan,  ambaye  alikuwa makamu  wake,  ajiuzulu, na  kwamba  atapambana  ili kurejea  madarakani. Nasheed  amewaambia  waungaji  wake  mkono   wapatao 2,000  kuwa  atarejea  madarakani  na  hatakubali mapinduzi  hayo. Na  baada  ya  hapo  aliongoza maandamano  mitaani. Polisi  walijibu  kwa  kufyatua mabomu  ya  kutoa  machozi  na  kuwakamata  wabunge wawili  kutoka  chama  cha  Nasheed.

Misri yashutumu NGO kwa kuingilia masuala ya ndani

Majaji  nchini  Misri  wanaochunguza  upataji  fedha  kutoka nje  kinyume  na  sheria  wa  mashirika  yasiyo  ya  kiserikali , wameyashutumu  makundi  ya  kigeni  na  ya  ndani  , ikiwa  ni  pamoja  na  yale  ya  Marekani  kwa  kuingilia kinyume  na  sheria  masuala  ya   kisiasa nchini  humo. Jaji  Sameh Abu Zeid  amewaambia  waandishi  habari  leo kuwa  baadhi  ya  mashirika  yasiyo  ya  kiserikali yanafanya kazi  bila  kibali , na  kazi  zao  zinahusiana moja  kwa  moja  na  masuala  ya  kisiasa na  sio  masuala ya  kijamii. Jaji  huyo  amesema  msako  uliofanywa  Desemba  mwaka jana  dhidi  ya  ofisi  17  za  mashirika  ya  ndani  na  ya kigeni, kama  sehemu  ya  uchunguzi  kuhusu  upatikanaji wa  fedha  kinyume  na  sheria  kwa  mashirika  hayo, ulifanywa  kwa  mujibu  wa  sheria. Watu  kadha wametakiwa  kufika  mahakamani  kwasababu kunaonekana  kuwa  na  ushahidi  wa  kutosha. Miongoni  mwao  ni  Wamarekani  19,  hali  iliyosababisha maseneta  watatu  wa   Marekani  kuionya  Misri   kuwa inajiweka  katika  hali  ya  kuvuruga  uhusiano  baina  ya mataifa  hayo  mawili.

Baraza la mawaziri launda tume ya majimbo kuchunguza uhalifu wa makundi yenye imani kali za mrengo wa kulia

Baraza  la  mawaziri  la  serikali  ya  Ujerumani   limeunda tume  ya  watu  wanne  ya  majimbo  itakayoshughulikia mauaji  yaliyofanywa  na  Wanazi  mamboleo. Tume  hiyo itafanya kazi  kwa  pamoja   na  vyombo  vya  usalama  vya majimbo  na  taifa, na   suala  kuu likiwa  ni kulilenga kundi  la  wanazimamboleo   la  Zwickau. Msingi   wa  tume hiyo  utakuwa  katika  matokeo  ya  ripoti  ya   uchunguzi iliyowasilishwa  katika  bunge  la  Ujerumani, Bundestag, na  bunge  la  jimbo  la  Thüringer. Wanazimamboleo wamehusika  katika  mauaji  ya  watu  tisa  ambao  ni wafanya biashara  wadogo,  wenye  asili  ya  Uturuki  na Mgiriki  mmoja  pamoja  na  polisi  mwanamke  mmoja. Suala  kuu ni   kwanini  maafisa  wa  idara  za  usalama  wa taifa  walishindwa   kuwagundua  watu  hao  waliofanya uhalifu  huo  ambao  ni  wenye  msimamo  mkali  wa mrengo  wa  kulia.

USA kupunguza ujumbe wake wa kidiplomasia nchini Iraq

Kwa  mujibu  wa  gazeti  la  New York Times , miezi  miwili baada  ya  kuondoa  majeshi  yake  kutoka  Iraq, Marekani inapanga  kuchukua  hatua  nyingine  muhimu ya kupunguza  kwa  kiasi  kikubwa   ujumbe  wake  wa kidiplomasia  nchini  humo. Katika  ubalozi  wa  Marekani mjini  Baghdad  kwa  hivi  sasa  kuna   wafanyakazi 16,000,   wanadiplomasia   2,000  na  wafanyakazi  wa kawaida  14,000, na  huenda  nusu  yao  wakaondolewa. Sababu  ya  kuchukuliwa   hatua  hii  ni  pamoja  na kuvunjika  moyo  kuhusiana  na  hali  ya  mkwamo  nchini Iraq  dhidi  ya  ushawishi  wa  Marekani  katika  hatua  za kidemokrasia  nchini  humo.  Uhusiano  usioridhisha hauhalalishi  gharama  inayofikia  kiasi  ya  dola  bilioni  sita kwa  mwaka  ambayo  Marekani  inakabiliana  nayo. Msemaji  wa  wizara  ya  mambo  ya  kigeni, Victoria Nuland,  amethibitisha  mpango  huo kwamba  Marekani inapanga  kuuwezesha  ujumbe  wa kibalozi  nchini  Iraq kufanyakazi  vizuri. Pamoja  na  hayo  haijafahamika   bado ni  kiasi  gani  ujumbe  huo  utapunguzwa.

Unaweza kusikiliza matangazo yetu hapa

Kusikiliza matangazo ya Idhaa ya Kiswahili ya DW, tafadhali bonyeza alama ya spika ya masikioni hapo chini, na kuwasiliana nasi, tafadhali tuandikie moja kwa moja kupitia: kiswahili@dw.de.

Maoni kutoka DW wiki hii yanajadili hatima ya kisiasa ya Kenya baada ya uamuzi wa ICC